
Na Mwandishi wetu
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeanza kuweka utaratibu wa kutumia hazina ya maarifa na uzoefu kutoka kwa Mabalozi Wastaafu ili kuimarisha utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuimarisha diplomasia ya nchi.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo , amebainisha utaratibu huo leo Aprili 15, 2026, jijini Dar es Salaam wakati anafungua kikao cha mashauriano kati ya uongozi wa Wizara na Mabalozi Wastafu.
"Wizara tumeanzisha utaratibu wa kuwa na vikao vya mara kwa mara na Mabalozi Wastaafu ili kuvuna maarifa na uzoefu wao kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia ili ulete nanufaa katika nyanja mbalimbali kama vile, siasa, ulinzi na usalama, uchumi, biashara, uwekezaji na utalii". Balozi Kombo alisema.

Balozi Kombo ametaja mifano ya maeneo ambayo angependa Mabalozi Wastaafu wachangie maarifa na uzoefu walio kuwa nao ili maeneo hayo yaendelee kuwa na manufaa zaidi kwenye nchi.
Maeneo hayo ni pamoja na mwenendo wa ufanyaji wa biashara baina ya Tanzania na nchi nyingine, hususan zilizopo barani Afrika.
Amesema utekelezaji wa Dira 2050 ambayo inalenga uchumi wa dola bilioni moja, ni eneo lingine muhimu ambalo maarifa ya Mabalozi Wastaafu yanahitajika ili kuhakikisha
utekelezaji wake unakuwa wa ufanisi.
Waziri Kombo ameongeza kuwa mabadiliko yanayoendelea duniani
hususan, maendeleo ya kidigitali yanahitaji mikakati thabiti ili nchi iweze kunufaika na kuwa na mipango madhubuti ya kukabiliana na athari zake. Haya yote yanahitaji mawazo ya pamoja ili kuyaendeea kwa ufanisi.
Eneo lingine ambalo Waziri Kombo alisisitiza umuhimu wa kupata uzoefu wa Mabalozi Wastaafu ni siasa za ulimwengu ambazo zimekuwa hazitabiriki na zinasababisha madhara mbalimbali, hususan katika nchi zinazoendelea kama Tanzania.
Aidha, uzoefu wa Mabalozi Wastaafu unahitajika katika kuendeleza na kuimarisha taswira nzuri ya nchi na hasa nchi inapopewa dhamana ya majukumu ya kimataifa. Balozi Kombo alisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika mwaka 2028 na hivyo maarifa yao ni muhimu ili kuhakikisha nchi inatekeleza jukumu hilo kwa ufanisi.
Awali, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alisema Wizara inaangalia uwezekano wa kuanzisha utaratibu rasmi kupitia Ofisi ya Rais-UTUMISHI ili ushirikishwaji wa Mabalozi Wastaafu uwe unatambulika rasmi.


No comments:
Post a Comment