MWENGE WAPONGEZA MRADI WA UFUGAJI NYUKI, KIKUNDI CHA TWIKONDELE YAFIKISHA MIZINGA 117 YA KISASA - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Sunday, 23 August 2026

MWENGE WAPONGEZA MRADI WA UFUGAJI NYUKI, KIKUNDI CHA TWIKONDELE YAFIKISHA MIZINGA 117 YA KISASA

 


Na Neema Nkumbi, KAHAMA

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, Wazo Michael Mwang’onda, ametoa pongezi kwa Kikundi cha Ufugaji Nyuki cha Twikondele kilichopo katika eneo la Bulyanhulu, Halmashauri ya Msalala, kwa kutumia ufugaji nyuki kama fursa ya kiuchumi huku kikichangia uhifadhi wa mazingira.


Kikundi hicho, kilichoanza na mizinga saba ya kienyeji, kwa sasa kina jumla ya mizinga 117 ya kisasa, baada ya kunufaika na ufadhili wa Sh milioni 25 kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Barrick Bulyanhulu mwaka 2023.


Fedha hizo zilitumika kununua mizinga 100 ya kisasa pamoja na kuwawezesha wanakikundi kupata maarifa ya ufugaji nyuki, hatua iliyowasaidia kuongeza uzalishaji wa asali na kuboresha maisha yao.


Esther Maziku Mayela, mwanakikundi, amesema ufugaji huo umemsaidia kupata kipato ambacho amekitumia katika kugharamia elimu ya watoto, kununua mifugo pamoja na kujenga nyumba.




“Kupitia ufugaji wa nyuki nimeweza kusomesha watoto, kununua mifugo kama mbuzi na kuku, pamoja na kujenga nyumba, Hii imekuwa fursa kubwa kwangu ya kuboresha maisha,” amesema Mayela.


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kikundi cha Twikondele, Beta Yawanga Ndeki, amesema mradi huo umeleta mabadiliko makubwa kwa wanakikundi, huku baadhi yao wakifanikiwa kusomesha watoto hadi ngazi ya chuo na kujenga nyumba bora.




“Tumefaidika sana na kikundi hiki. Tumeweza kusomesha watoto wetu, wengine wako chuoni na wengine wameshamaliza, tumejenga nyumba bora na kununua mifugo, Tunashukuru kwa kuwezeshwa kuwa na mizinga 117,” amesema Yawanga.


Amesema katika msimu mmoja wa uzalishaji mwaka huu, kikundi kimefanikiwa kuvuna takribani lita 200 za asali, ikilinganishwa na lita 60 walizokuwa wakizalisha awali.


Mwanakikundi mwingine, Rehema Daniel, amesema kupitia kikundi hicho wameweza kufungua akaunti ya pamoja, kuanzisha shughuli za ufugaji kuku na kununua eneo kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya kikundi.


Akizungumza kuhusu uwezeshaji huo, Kiongozi wa Kitengo cha Mahusiano na Jamii ya Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, Zwena Semkondo, amesema mgodi huo umeendelea kushirikiana na jamii katika miradi ya maendeleo, ikiwemo kuwawezesha wanakikundi cha Tikondele katika ufugaji nyuki.




“Tumeweza kuwezesha kikundi cha Tikondele kwa kutoa mizinga ya kisasa, kuanzia mafunzo hadi uzalishaji, Hadi sasa baadhi ya wanakikundi wameanza kuzalisha na mapato wanayopata yameendelea kuwasaidia katika shughuli mbalimbali za maendeleo, ikiwemo kusomesha watoto na kujenga nyumba bora,” amesema Semkondo.


Amesema Barrick Bulyanhulu inalenga kuendeleza mradi huo kwa kuongeza uzalishaji wa asali na mazao mengine yatokanayo na ufugaji nyuki, huku akisisitiza kuwa shughuli hiyo ina mchango mkubwa katika uhifadhi wa mazingira.


Mkimbiza mwenge kitaifa amekipongeza Kikundi cha Twikondele kwa kuanzisha kuotesha vitalu vya miti ya matunda, ikiwemo michungwa, ambavyo miche yake huuzwa kwa wananchi kwa ajili ya kupandwa katika maeneo mbalimbali.


Mwang'onda amesema hatua hiyo inaendana na juhudi za Serikali za kutunza mazingira, akimtaja Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuwa kinara wa uhifadhi wa mazingira na matumizi ya nishati safi na salama.


Aidha, amewataka wananchi wa Msalala kuendelea kutunza mazingira kwa kupanda miti rafiki kwa mazingira, hususan katika maeneo yanayozunguka vyanzo vya maji.




“Tuendelee kuhifadhi na kutunza mazingira yetu Kila mmoja katika eneo lake apande miti rafiki kwa mazingira na tuhakikishe tunalinda vyanzo vya maji, Tunahitaji miti ambayo itasaidia kuhifadhi maji na wakati huo huo kutupatia faida kupitia matunda,” amesema.


Amesema mfano wa Kikundi cha Twikondele, ambacho kimeunganisha ufugaji nyuki na uoteshaji wa miti ya matunda, unapaswa kuigwa na jamii nyingine katika jitihada za kulinda mazingira huku wakijipatia kipato.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso