SAUTI YA WAZEE: AMANI HUANZIA MOYONI, SIO SERIKALINI - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Friday, 14 November 2025

SAUTI YA WAZEE: AMANI HUANZIA MOYONI, SIO SERIKALINI



WACHAMBUZI wa masuala ya kisiasa na jamii wamesema mchango wa wazee katika kudumisha utulivu baada ya taharuki za kisiasa ni wa muhimu na wa kutilia mkazo.

Mwandishi mmoja wa makala ya kijamii aliandika, 'Sauti yao ni ngome ya busara na heshima ambayo inaweza kubadilisha jamii kuliko mamlaka yoyote.' Kauli hii inaonyesha umuhimu wa kuwasikiliza na kuwawezesha wazee kushiriki kikamilifu katika malezi ya kijamii.

Aidha inafaa ikumbukwe kuwa kila jamii imara imejengwa juu ya msingi wa hekima, na hekima hiyo mara nyingi hutoka kwa wazee. Wazee ni hazina ya taifa, walinzi wa maadili, na walimu wa vizazi vipya. Tanzania, taifa linalojivunia mila za heshima na utu, lina wajibu wa kuendelea kuthamini sauti zao, hasa katika kipindi hiki cha kujenga upya amani na maridhiano baada ya changamoto za kisiasa.

Wazee wanahimizwa kukaa na vijana, wazungumze nao kwa upendo na subira kuhusu thamani ya kulinda mali za umma na binafsi.

"Wazee wa taifa hili wametumia maisha yao kulinda amani, wakijitolea katika vita, kazi, na ujenzi wa uchumi. Ni haki yetu kusikiliza ushauri wao, kwa sababu wameona mengi kuliko sisi," inasema sehemu ya makala hiyo.

" Amani haianzi serikalini, bali inaanzia mioyoni mwa watu. Kama wazazi na walezi, tuna jukumu la kujenga kizazi kinachoamini katika busara badala ya hasira, mazungumzo badala ya makabiliano, na heshima badala ya chuki" anasema Franklin Leonard wa Morogoro.

Mama Mary Nyerere, mwalimu mstaafu, anaeleza: “Elimu ya amani inaanzia nyumbani. Mtoto akiona wazazi wanaheshimiana, atajifunza heshima. Akiona upendo, atajifunza upendo.”

Wazee wanapaswa kuwakumbusha vijana kuwa mali ya umma kama barabara, shule, hospitali, na ofisi za Serikali si mali ya chama, bali ni mali ya wananchi wote. Uharibifu wake ni sawa na kuchoma nyumba ya familia nzima.

Kwa mujibu wa wataalamu wa jamii, mabadiliko ya kimaadili yanapaswa kuanza katika familia. Mtoto anayejifunza thamani ya maisha ya wengine hawezi kushiriki katika kuharibu mali za umma au binafsi.

Katika tamaduni nyingi za Kiafrika, wazee wamekuwa walinzi wa mila na desturi, wapatanishi, na washauri wa uongozi. Heshima kwa wazee ni heshima kwa taifa. Tukianza kuwapuuza, tunapoteza dira ya maadili.

Leo, wazee wanahimizwa kutumia nafasi zao za kijamii kuwa walimu wa maadili, wakiwakumbusha vijana kwamba: “Kuhifadhi mali za umma na binafsi si kazi ya Serikali pekee, ni jukumu la kimaadili linalotufanya sisi wote kuwa walinzi wa maendeleo yetu.”

mwisho

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso