MUDA HAUJAFIKA KUWASEMA VIBAYA KOCHA MAKI NA MSHAMBULIAJI DEJAN WA SIMBA - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Wednesday 17 August 2022

MUDA HAUJAFIKA KUWASEMA VIBAYA KOCHA MAKI NA MSHAMBULIAJI DEJAN WA SIMBA


NI vigumu sana kwangu kuamini kwamba Simba wanaweza kuwa wamekosea sana kumpeleka kwao kocha Maki baada ya mchakato wa nguvu wa kumpata. ANAANDIKA IBRAHIM MKAMBA.


Ni wazi Maki ni mmoja wa makocha wakubwa na wazuri. Bahati mbaya kwetu soka, nikiazima maneno ya mtaalam Amri Kiemba, ni kama chumvi kwenye mboga, ukiiweka tu inakolea papo hapo. Tunalazimisha mafanikio ya haraka kwenye soka kama chumvi kwenye mboga!


Ni miezi isiyofikia 18 nyuma, watu kadhaa wa Yanga walifikiria kumpa kocha Nabi idadi ya mechi za kushinda kabla ya kumfukuza wakati yeye alisisitiza alikuwa akiijenga timu kimuunganiko. Leo hii Yanga hao hao wanamwita kocha Nabi Profesa kwa ujuzi mkubwa alionao wa kazi yake. Amewapa mafanikio mengi makubwa.


Je angetimuliwa kwa kutaka kwetu soka ikolee haraka kama chumvi kwenye mboga, Yanga si ingekosa leo kunufaika na ujuzi wa Nabi usio wa kawaida?


Uchebe akiwa kocha wa Simba alipigiwa kelele kubwa na mashabiki wa Simba kutaka atimuliwe na timu aachiwe Masud Djuma! 


Kilichofuata baadaye, baada ya Uchebe kuivusha Simba kwenye hatua ya makundi ligi ya mabingwa Afrika mbele ya matimu magumu mno, mzungu huyo anatukuzwa mno Simba mpaka leo. 


Leo hayo hayo ya Uchebe yanamkuta Maki. Kushindwa mechi moja tu dhidi ya timu kubwa, ambayo naomba msamaha kueleza ni kubwa kuliko hiyo Simba, tena kwa tofauti ya goli moja tu, tayari kuna kelele kuwa kocha hafai, afukuzwe! Hivi Yanga na Simba zikicheza lazima Simba ishinde? 


Je hatuujui ukweli kwamba kihistoria Yanga haishindwi sana na Simba kwa maana ya yenyewe kushinda au mechi kuisha kwa sare? 


Je watu hao wa Simba wangekuwa kwenye hali gani kama wao kwa Yanga wangefungwa 6-0 chini ya Mwalimu Nyerere, 4-1 chini ya Mzee Ruksa Alhaji Ali Hassan Mwinyi, 4-1 chini ya Mzee Mkapa,  5-0 chini ya Alhaji Jakaya Kikwete na 4-1 chini ya muda mfupi wa Dkt John Pombe Magufuli?
 

Mbona Wananchi wana raha sana na timu yao bila kujali kuwepo kwa kumbukumbu mbaya kama hizo? Ingekuwaje majuzi Simba ingepigwa 3-1 ambazo ziliwezekana? Si watu wangetaka hata Try Again atimuliwe?


Naomba watu watunze post hii. Utafika wakati Maki ataitwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kutokana na makubwa atakayowafanyia Simba. Na huyu mzungu Dejan anayeambiwa si lolote atageuka kipenzi cha Wana Simba kwa kufunga karibu kila mechi zikiwemo hat-trick kadhaa.
 

Hapo kuna watu wataabika kwa kejeli zao za leo kwa Waserbia hao wawili. Time will tell brothers and sisters. 

1 comment:

  1. Unavyosema kubwa timu kubwa angalia caf club rank ndio utaelewa nani mkubwa ,we unaandika tu

    ReplyDelete

Post Top Ad

Pages

Huheso