WIKI YA UTUMISHI WA UMMA YASOGEZA HUDUMA ZA TAASISI ZA UMMA KARIBU NA WANANCHI - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Wednesday, 24 June 2026

WIKI YA UTUMISHI WA UMMA YASOGEZA HUDUMA ZA TAASISI ZA UMMA KARIBU NA WANANCHI

 



Na Mwandishi Wetu - Dodoma


Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2026 yameonesha kwa vitendo namna taasisi za umma zinavyoendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kutumia majukwaa mbalimbali ya utoaji huduma, elimu na utatuzi wa changamoto.

Kupitia maonesho hayo, maelfu ya wananchi walipata huduma mbalimbali, elimu na ufumbuzi wa changamoto zao katika eneo moja.

Maadhimisho hayo yaliyofanyika kuanzia Juni 16 hadi 23, 2026 katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, yalizikutanisha taasisi za umma kutoka sekta mbalimbali chini ya kaulimbiu isemayo: “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu.”

Akizungumzia ushiriki wa Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) na taasisi za umma katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano kwa Umma na Mawasiliano wa Ofisi hiyo, Bw. Sabato Kosuri, alisema Wiki ya Utumishi wa Umma imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuonesha namna taasisi za umma zinavyowajibika kwa wananchi kwa kusogeza huduma karibu na wananchi, sambamba na kutoa fursa ya kupata elimu, ushauri na ufumbuzi wa changamoto katika eneo moja.

Alisema OTR, kwa kushirikiana na taasisi za umma zilizo chini ya usimamizi wake, ilitumia maadhimisho hayo kutoa elimu kuhusu majukumu ya taasisi hizo, kupokea maoni ya wananchi, kujibu maswali yao na kusogeza huduma mbalimbali karibu na walengwa.

Aidha, alibainisha kuwa hatua hiyo inaakisi mwelekeo wa Serikali wa kuimarisha utoaji wa huduma kwa kutumia mifumo ya kidijitali na kuongeza uwajibikaji katika sekta ya umma.

“Maadhimisho haya yamethibitisha kuwa taasisi za umma hazisubiri tena wananchi kufika ofisini. Kupitia ushiriki wa OTR na taasisi zinazosimamiwa na Ofisi yetu, wananchi wameweza kupata huduma, elimu na majibu ya changamoto zao kwa wakati, jambo linaloimarisha uhusiano kati ya Serikali na wananchi,” alisema.

Katika maadhimisho hayo, Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) ulitoa vyeti vya kuzaliwa 750 kwa utaratibu wa ndani ya siku moja badala ya muda wa kawaida wa siku mbili, huku pia vyeti 10 vya vifo vikitoa kwa haraka.

Afisa Sheria wa RITA, Bi. Emmanuela Mwingira, alisema zaidi ya wananchi 1,000 walipata elimu kuhusu wosia, usajili wa ndoa na masuala ya bodi za wadhamini.

“Maadhimisho haya yamewarahisishia wananchi kupata huduma kwa wakati na kuwapunguzia safari za kufika ofisini,” alisema Bi. Mwingira.

Kwa upande wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Meneja Masoko, Bw. Fredrick Kalinga, alisema zaidi ya wananchi 1,500 walitembelea banda lao na kupata elimu ya vitendo kuhusu uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme.

Aliongeza kuwa wananchi pia walipatiwa elimu kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa NIKONEKTI, unaorahisisha huduma kwa wateja wapya kwa kupunguza gharama, muda wa kusubiri na urasimu wakati wa kuomba huduma za kuunganishiwa umeme.

Aidha, walipata elimu kuhusu magari yanayotumia umeme, usalama wa matumizi ya umeme, pamoja na huduma kwa wateja kupitia namba ya bure 180 inayopatikana saa 24.

“Tulitumia maadhimisho haya kujibu maswali ya wananchi, kupokea maoni yao na kutatua changamoto mbalimbali zinazohusu huduma za umeme,” alisema Bw. Kalinga.


Sekta ya afya nayo haikubaki nyuma

Afisa Rasilimali Watu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Hilda Kajia, alisema katika kipindi cha siku nane waliwahudumia wananchi 260 kwa uchunguzi wa magonjwa ya ngozi, macho na ushauri wa afya ya uzazi na magonjwa ya wanawake bila malipo.

Alisema huduma hizo zisingepatikana kwa urahisi bila maadhimisho hayo, ambayo yamewarahisishia wananchi kupata huduma bila kupitia taratibu za kawaida za hospitali.

Nayo Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliwahudumia wananchi 720 kwa vipimo vya shinikizo la damu, sukari, mafuta kwenye damu pamoja na uchunguzi wa moyo.

Meneja wa Huduma za Utawala wa JKCI, Bw. Joachim Asenga, alisema baadhi ya wananchi waliobainika kuwa na changamoto za kiafya walipewa ushauri, kuanzishiwa matibabu na kupewa rufaa, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kuepuka madhara makubwa ya magonjwa ya moyo.

"Tumewasaidia wananchi kuwa na elimu sahihi ya magonjwa ya moyo ili wapate matibabu kabla ya athari kujitokeza," alisema huku akitoa wito kwa wananchi kutoacha kupima afya zao.

Aliongeza: “Huduma zote kwa hapa kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yametolewa bure.”

Kwa upande wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Afisa Uhusiano na Mawasiliano Mkuu, Bi. Theresa Chilambo, alisema zaidi ya wananchi 720 walitembelea banda lao, huku wateja wapya 400 wakianza mchakato wa kurasimisha biashara zao kupitia mfumo wa BRELA Online System ulioanza kutumika Aprili 8, 2026.

Bi. Chilambo alisema maadhimisho hayo yameongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kurasimisha biashara, akibainisha kuwa mfumo huo mpya unalenga kuondoa mianya ya upatikanaji wa huduma kupitia watu wa kati ‘vishoka’, kwa kuwa usajili unafanywa na wakurugenzi na wanahisa pekee wenye mamlaka ya kufikia mfumo huo.

Nayo Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) iliwahudumia wananchi 157, huku wateja wapya 26 wakipatiwa huduma ya maji.

Afisa Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Bi. Halima Kambi, alisema pia wananchi walipata elimu kuhusu mfumo wa e-Mrejesho unaowawezesha kulipa bili na kutoa malalamiko mtandaoni bila kufika ofisini, akieleza kuwa lengo ni kuhakikisha huduma zote muhimu zinapatikana kidijitali ili kuokoa muda na gharama.

Maadhimisho hayo yameonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi kupitia uwezeshaji wa kidijitali, kuongeza uwajibikaji wa taasisi za umma na kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana kwa urahisi zaidi bila wananchi kulazimika kusafiri umbali mrefu.

Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yalifunguliwa rasmi na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, Juni 17, 2026, na kufungwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Moses Kusiluka.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso