▪️Awataka kuharakisha utekelezaji wa mradi na malipo ya fidia kwa wananchi
▪️Faru Graphite waahidi kuendelea na kazi za awali za ujenzi baada ya kupisha msimu wa mvua
▪️Ni mradi mkubwa wa Madini Kinywe utakaochochea ukuaji wa uchumi Mkoani Morogoro
📍 Dar Es Salaam
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Peter Mavunde amesisitiza na kuwataka wawekezaji wote wa miradi ya uchimbaji madini kuanza utekelezaji wa miradi hiyo haraka ili kuchochea ukuaji wa sekta na pato la Taifa nchini.
Ameyasema hayo leo tarehe 19 Juni, 2026 katika Ofisi ndogo za Wizara ya Madini Jijini Dar es Salaam alipokutana na uongozi wa Kampuni ya Faru Graphite Corporation ambao wapo mbioni kuanza utekelezaji wa mradi wa uchimbaji madini kinywe Wilayani Mahenge, Mkoani Morogoro.
"*Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan* ameendelea kuwa kinara kwa kuweka mazingira rafiki yanayovutia na kurahisisha uwekezaji nchini Tanzania. Hili linaonekana wazi kwa miradi mingi ya wawekezaji iliyopo na ambayo ipo mbioni kuanza utekelezaji wake"
Amesema ni muda muafaka sasa kwa wawekezaji wote kwenye sekta ya madini ambao miradi yao haijaanza utekelezaji kuunga mkono jitihada hizi za Mheshimiwa Rais kwa vitendo na kuanza haraka utekelezaji wa miradi hiyo ili ilete tija kwa Taifa.
Aidha, Waziri Mavunde ametoa wito kwa uongozi wa Faru Graphite kuhakikisha wanaharakisha kuanza utekelezaji wa mradi wao wa uchimbaji madini kinywe Wilayani Mahenge ikiwa ni pamoja na ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaopisha utekelezaji wa mradi huo.
Waziri Mavunde pia ameeleza kuwa, mradi huo mkubwa wa uchimbaji madini kinywe utakaodumu kwa takribani miaka 26 utasaidia kuzalisha ajira na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Morogoro na Taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Black Rock Limited, *Bw. John De Vries* ameishukuru Serikali kwa namna inavyowapa ushirikiano katika utekelezaji wa mradi huo na kuahidi kuwa Faru Graphite ipo tayari kuendelea na kazi za awali za ujenzi wa mradi huo baada ya msimu wa mvua kuisha ambao ulikuwa ni changamoto kwao.






No comments:
Post a Comment