Mkazi wa Nyashimbi Manispaa ya Kahama, Bw. Bakari Kipindula, ametoa wito kwa wananchi wenzake kuendelea kuilinda na kuitunza amani ili jamii iweze kuendelea na shughuli za maendeleo bila hofu wala vurugu.
Akizungumza kuhusu hali ya kijamii na maendeleo, amesema licha ya changamoto zilizowahi kujitokeza katika vipindi mbalimbali vya uongozi, bado wananchi wanapaswa kuweka mbele mazungumzo, mshikamano na utulivu kama njia ya kudumisha umoja.
Amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na kuepuka kushawishiwa vya kuingia kwenye vitendo vinavyoweza kuvuruga amani na usalama wa Taifa kwa ujumla.
Aidha, ameiomba serikali kuhakikisha watendaji wake wanawasikiliza wananchi, kutatua kero zao kwa wakati na kutenda kwa uadilifu, akieleza kuwa baadhi ya migogoro huanza pale changamoto za wananchi zinapopuuzwa.
Bw. Kipindula amesema amani ikidumu italeta tija kwa uchumi wa taifa na maendeleo ya jamii, huku akionya kuwa matukio ya vurugu na uharibifu huathiri wananchi wote pamoja na serikali.
Katika hitimisho lake, amewataka wananchi kuungana, kupinga uchochezi, na kuendelea kujenga taifa lenye utulivu na maendeleo, huku akiishukuru serikali kwa juhudi mbalimbali za kuwaletea wananchi maendeleo.

No comments:
Post a Comment