ELIMU YA FEDHA KUIBUA MABADILIKO YA KIFEDHA KIGOMA - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Sunday 9 June 2024

ELIMU YA FEDHA KUIBUA MABADILIKO YA KIFEDHA KIGOMA





Serikali imewataka wananchi kufanya maamuzi mazuri ya matumizi ya kifedha kulingana na malengo waliyojiwekea, ikiwemo kuweka akiba, kupanga matumizi, na kudhibiti deni, ili kuepuka changamoto za kifedha wanazokumbana nazo na kujenga ustawi wao kibinafsi.


Akizungumza na wananchi wa Nyachenda, Afisa Usimamizi wa Fedha katika Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha katika Wizara ya Fedha, Bi. Grace Samwel, alisema kuwa Kupitia elimu ya fedha, wananchi wanaweza kujifunza njia za kuongeza mapato yao, kuwekeza kwa busara, na kuanzisha biashara zinazofaa.


“Hii inaweza kusaidia kupunguza umaskini kwa kutoa fursa za kifedha na kuchochea ukuaji wa uchumi wa kijamii” alisema Bi. Grace Samwel


Alisema kuwa elimu ya fedha inawawezesha wananchi kuelewa hatari za kifedha na jinsi ya kuzikabili akitolea mfano wa kuwaelimisha umuhimu wa kukata bima na kujiandaa na matukio yasiyotarajiwa kama vile magonjwa au majanga ya asili.


“Wananchi walio na uelewa mzuri wa fedha wanaweza kuchangia kwa njia mbalimbali katika maendeleo ya jamii yao kwa kufanya uwekezaji unaostahili katika elimu, afya, miundombinu, na miradi mingine ya maendeleo, hivyo kusaidia kuinua kiwango cha maisha ya jamii yao kwa ujumla” Alisema Bi. Grace Samwel


Kwa upande wake Afisa Usimamizi wa Fedha, Wizara ya Fedha, Bw. Stanley Kibakaya, alisema kuwa elimu ya fedha wanayoitoa inawawezesha wananchi kutumia pesa zao vizuri, lakini pia ni zana ya kuwawezesha kujenga maisha yenye msingi imara wa kifedha na kuchangia katika maendeleo ya jamii yao kwa ujumla.


Naye Afisa Kilimo wa Mkoa wa Kigoma, Bw. Amiri Kasali, aliishukuru Wizara ya Fedha kwa jitihada zake za kuendelea kutoa elimu ya fedha mkoani Kigoma kutokana na umuhimu wake, kwani inawawezesha kufanya maamuzi sahihi kuhusu fedha zao na maisha yao kwa ujumla.


" Kupitia elimu hii, wananchi wanaweza kujifunza jinsi ya kuweka akiba, kupanga matumizi, kuwekeza, na hata kujua njia bora za kujikwamua kiuchumi na kibiashara. Hii inasaidia sana katika kuongeza ustawi na maendeleo ya jamii ya Kigoma kwa ujumla. ". Alisema Bw. Kasali


Bw. Evarist Kamwele, ni mmoja wa wananchi wa Kata ya Nyachenda, Mkoani Kigoma, ambaye alinufaika na elimu ya fedha inayotolewa na Wizara ya Fedha na kueleza kuwa elimu hiyo imeweza kubadilisha mtazamo wake kuhusu fedha na kumfungua macho yake kuhusu umuhimu wa kufanya maamuzi sahihi linapokuja suala la matumizi na uwekezaji.


Alisema kuwa kabla ya kupata elimu hiyo, yeye pamoja na wengine wengi walikuwa hawatilii maanani sana jinsi wanavyotumia pesa zao au wanavyochukua mikopo, jambo ambalo lilisababisha matatizo ya kifedha na hata madeni yenye riba kubwa kwa baadhi yao.


“Lakini baada ya kupitia mafunzo ya fedha yaliyotolewa na Wizara ya Fedha, nimepata ufahamu mpya na uelewa wa kina juu ya mambo kama akiba, uwekezaji, mipango ya kifedha, na hata jinsi ya kuepuka madeni mabaya” aliongeza Bw. Kamwele.


Wizara ya Fedha, kwa kushirikiana na wadau wengine inaendelea na kampeni ya kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya fedha katika mikoa mbalimbali nchini ikiwa ni utekelezaji wa mpango mkakati wake wa Mpango mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya 2020/21 - 2029/30.


Lengo kuwa ifikapo mwaka 2025, asilimia 80 ya watu nchini wawe na uelewa wa masuala ya fedha.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso