META KUWAPATIA VIFAA WACHIMBAJI WADOGO - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Tuesday 30 April 2024

META KUWAPATIA VIFAA WACHIMBAJI WADOGO


Mwakilishi kutoka Kampuni ya META Mha. Issa Mndeme amesema wapo katika hatua ya utiaji saini ya makubaliano ya ukodishaji na uuzaji vifaa vya uchimbaji kwa wachimbaji wadogo ili kuwasaidia kuepukana na changamoto mbalimbali ambazo wamekuwa wakikumbana nazo kwenye uchimbaji.

Mha. Mndeme ameyamesema hayo Jijini Dodoma kwenye mkutano wa kamati tendaji na Halmashauri kuu ya Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini (FEMATA) katika utiaji saini wa makubaliano ya ukodishaji na uuzaji vifaa vya uchimbaji kwa wachimbaji wadogo kati ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na META.

Amesema kampuni yao ikijihusisha na usambazaji pamoja na kuuza vifaa vinavyotumika katika uchimbaji madini, ujenzi na kazi zinazohusisha mashine kubwa.


“Kampuni ya META ipo chini ya kampuni ya Meta Group Africa inayofanya kazi katika nchi 7 Afrika ikiwemo Tanzania, Rwanda, Uganda, Kenya, Angola, Msumbiji na Zambia”,amesema.

Akizungumza kwenye mkutano huo Waziri wa madini Mhe. Anthony Mavunde ameahidi kufuta leseni za tafiti ambazo hazifanyiwi kazi ili kuweza kuepusha unyanyasaji wa wachimbaji wadogo unaowapelekea kuonekana ni watumwa katika nchi yao.

“Kilio chetu ni kwamba mnapoteza mitaji na nguvu nyingi sana kwa kuchimba kwa kubahatisha, hivyo serikali haiwezi kukwepa jukumu la kimsingi kabisa kupitia tafiti na bahati mbaya sana tuliambiwa kiwa tafiti ni gharama serikali itaweza kuwasaidia”, amesema.

Amesema ni jukumu la serikali kuwaongoza wachimbaji wa madini katika njia sahihi za uchimbaji kupitia tafiti bila kujali gharama.

Aidha Mavunde ameongeza kuwa kwa mwaka wa fedha uliopita 2022/23 mchango wa sekta ya madini katika pato la taifa ilikuwa bilioni 678 ya mchango wa wachimbaji wadogo.

Kwa upande wake Rais wa FEMATA John Bina amesema vyama hivyo vinaendelea kushirikiana na serikali kupitia tume ya madini ili kuhakikisha uchimbaji salama pamoja na kupatia wachimbaji wadogo vitambulisho.

Amesema malengo yao ni kuona wachimbaji wadogo wanapiga hatua kutoka kwenye uchimbaji mdogo kwenda hatua ya kati hadi uchimbaji mkubwa.

“Jina la FEMATA limepewa maono na Mhe. Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan na kuiona Tanzania inanufaika na kampuni yetu kupitia kodi, FEMATA inaendelea kuwahamasisha wachimbaji wenzetu kuhusu umuhimu wa kulipa kodi na kuishahuri serikali ili TRA iwe inatoza kiwango cha 2% ya kodi ya mapato kwa wachimbaji wadogo kwa madini yote,”amesema.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso