WAZIRI MKUU AZINDUA RIPOTI YA MPANGO WA MATUMIZI BORA YA ARDH YA KIJIJI - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Friday 22 March 2024

WAZIRI MKUU AZINDUA RIPOTI YA MPANGO WA MATUMIZI BORA YA ARDH YA KIJIJI

WAZIRI MKUU wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa leo Machi 22, 2022 amezindua ripoti ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi ya Vijiji Wilayani Ruangwa mkoni Lindi, uzinduzi ambao umeenda sambamba na utoaji wa vyeti 18 vya ardhi ya Kijiji.


Waziri Mkuu amefanya uzinduzi huo katika Mkutano wa Wadau Kujadili Utekelezaji Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi, uliohusisha wadau mbalimbali wa masuala ya ardhi kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Ruangwa.


Waziri Mkuu ameeleza kuwa Lengo la Serikali ni kupima ardhi yote nchini ili wananchi wakiwepo wanavijiji waweze kuitumia katika kufanya shughuli za kiuchumi.


Amewaagiza Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi ambao Halmashauri zao zinafikiwa na mradi kuhakikisha kuwa wanashirikiana na Wizara ya Ardhi katika kufanikisha mradi huo.


“Nisisitiza Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Wenyeviti na Watendaji katika vijiji washiriki kikamilifu kuwafikia wananchi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa matumizi sahihi ya ardhi, ili waweze kunufaika pamoja na kupata hati milki za ardhi wanayoimiliki”

Waziri Mkuu pia amesema juhuhudi zinazofanyika katika upimaji wa ardhi nchini ni matokeo ya utendaji kazi na usimamizi mzuri unaofanywa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.


“Mhe. Rais amekuwa mstari wa mbele katika kusisitiza juu ya upimaji wa ardhi, hata nilipomuambia nakuja huku amenipa salamu zenu na anafuatilia hiki kinachondelea kupitia vyombo mbalimbali vya habari na Serikali yake itaendelea kutenga bajeti kwaajili ya kazi ya upimaji”


Awali, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geofrey Pinda, alisema mradi huo utavifikia vijiji vyote katika wilaya ya Ruangwa, ili kuhakikisha kuwa mpango wa matumizi bora vijijini unapata mafanikio makubwa.


Amesema kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazokabiliwa na kasi kubwa ya ukuaji wa miji na vijiji kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu linalosababisha kuongezeka kwa mahitaji ya ardhi iliyopangwa na yenye usimamizi mzuri na salama.


“Wizara imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali kukabiliana na changamoto hizi kwa kufanya maboresho mbalimbali ya huduma za Sekta ya Ardhi, kuhuisha miundo ya Wizara na kubuni programu na miradi mbalimbali kama vile programu ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha na Programu ya Urasimishaji wa Makazi yaliyojengwa kiholela”. Alieleza Mhe. Pinda


Ameongeza kuwa Kutokana na mahusiano mazuri ya kidiplomasia yaliyowekwa na Serikali yetu ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania na mashirika ya kimataifa pamoja na nchi mbalimbali Duniani, Tanzania tumefanikiwa kusaini Mkataba na Benki ya Dunia wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 150 kwa ajili ya kuboresha Usalama wa Milki za Ardhi nchini.


“Mradi huu unaofadhiliwa na benki ya dunia ni wa kwanza kupata fedha nyingi katika sekta ya ardhi ya Dunia Kusini mwa Jangwa la Sahara, Wizara tunaahidi kusimamia vizuri utekelezaji wa mradi huu ili kuendelea kuiweka nchi yetu kwenye taswira nzuri kimataifa,” alisisitiza.


Akitoa salamu za wananchi wa Ruangwa kwa mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Hassan Ngoma ameishukuru Serikali kwa juhudi inazozifanya katika kushughulikia masuala ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo wilaya ya Ruangwa hali ambayo inaenda kumaliza changamoto zinazowakumba wananchi.


Aidha alitumia nafasi hiyo kutoa rai kwa viongozi kuendelea kuusimamia Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) ili ulete tija katika jamii.


Mradi wa Uboreshaji wa Usalama wa Milki za Adhi (LTIP) unasimamiwa na Wizara ya Adhi Nyumba na Mandeleo ya Makazi ukiwa na kauli mbiu isemayo; “Usawa wa Kijinsia katika Umiliki wa Ardhi katika Ustawi wa Jamii”.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso