MKURUGENZI WA HALMASHAURI, MTENDAJI NA MWENYEKITI WA KIJIJI WAKATALIWA NA WANANCHI KWA TUHUMA YA UFUJAJI WA FEDHA ZA KIJIJI - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Thursday 5 January 2023

MKURUGENZI WA HALMASHAURI, MTENDAJI NA MWENYEKITI WA KIJIJI WAKATALIWA NA WANANCHI KWA TUHUMA YA UFUJAJI WA FEDHA ZA KIJIJI

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida, Jeshi Lupembe akizungumza kwenye mkutano huo.

Taswira ya mkutano huo.


WANANCHI wa Kijiji cha Manga Kata ya Ntipa Manispaa ya Singida wamewakataa viongozi wa kijiji hicho akiwamo Mwenyekiti na Mtendaji wa kijiji mbele ya Mbunge wa Singida mjini, Mussa Ramadhani Sima na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa Singida, Jeshi Lupembe wakiwatuhumu mambo kadhaa ikiwamo ufujaji wa fedha za kijiji.


Wananchi hao waliwakataa viongozi wao na kumtaka Mkurugenzi na Mbunge waondoke nao hawawataki kuwaona katika kijiji hicho wakati wa mkutano wa hadhara ulioitishwa na mbunge.


Mbunge aliitisha mkutano huo Januari 3, 2023 baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi kwamba Mtendaji aliyetajwa kwa jina la Reuben Njou amewachangisha maelfu ya fedha kwa ajili ya ujenzi wa vyoo vya Shule ya Sekondari mpya ya kijiji hicho kinyume na utaratibu.


Katika mkutano huo Mbunge Sima aliamuru fedha hizo warudishiwe mara moja wananchi 18 waliotoa Sh.30,000 kila mmoja kati ya wananchi 124 waliotakiwa kuzitoa huku akichukua hatua ya kutoa fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa vyoo hivyo vya wanafunzi vyenye matundu nane ambao umekuwa ukiendelea kwa kasi.


Afisa Mtendaji huyo, Reuben Njou alipoulizwa kuhusu tuhuma hizo alisema sio za kweli na kuwa jambo hilo lipo kisiasa zaidi kwani mchakatowake ulifanyika baada ya kufanyika kwa vikao vya kamati ya maendeleo ya kata hiyo na halmashauri ya kijiji.


Alisema vikao hivyo viliwashirikisha wazazi wa wanafunzi waliofaulu ambao walikubali kuchangia Sh.30, 000 ambapo wazazi 13 kati ya 103 ndio walitoa kiasi hicho lakini wengine walitoa chini hapo na jumla ya fedha zilizopatikana zilikuwa ni Sh.503,000 fedha zilizotumika kunua saruji, mchanga, maji na kumlipa fundi.


Alisema mchanganuo mzima ma suala hilo upo kimaandishi na wala hauna shida kabisa na akasema sakata hilo limetengenezwa na viongozi wastaafu wa kijiji hicho ambao wanataka kurudi madarakani.


Baadhi ya kero zilizotolewa na wananchi hao katika mkutano huo ni ubadhirifu wa fedha za mradi wa ujenzi wa daraja ambapo viongozi wa kijiji hicho waliingia mkataba na mkandaras wa kubeba mawe kutoka eneo la kijiji tripu 33 na wao kudai ni tripu 10 kwa malipo ya Sh.100,000 wakati sio kweli na baadae kuwataka wananchi kufanya kazi ya kubeba mawe hayo hadi lilipokuwa likijengwa daraja hilo.


Madai mengine yaliyoibuliwa ni ubadhirifu katika ukusanyaji wa mapato katika mdana wa kijiji hicho ambapo walimuomba Mkurugenzi kuwaweka watu wengine ili kubaini makusanyo yanayokusanywa ambayo yatakuwa tofauti na yale yanayokusanywa.


Kero nyingine iliyoibuliwa dhidi ya Afisa mtendaji huyo ni kujifanya ni Mungu mtu kutowasikiliza wananchi na katika mikutano ajenda zote kuziendesha yeye bila ya kuwahusisha wajumbe.


“Mkurugenzi huyu mtendaji ni muajiriwa wa ofisi yako unaweza kumpa kazi hata ya kupanga mafaili katika ofisi yako tunaomba uondoke naye sisi hatumtaki hapa kijijini” alisema mmoja wa wakazi wa eneo hilo.


Kero nyingine iliyotolewa katika mkutano huo ilihusu namna ya utoaji ajira za muda mfupi kama wakati wa chanjo na sensa ya watu na makazi ambapo vijana wengi waliopata fursa hiyo walikuwa ni ndugu na jamaa wa watumishi wa serikali ambapo vijana wa maeneo hao hawakupata fursa hiyo.


Baada ya kupokelewa kwa kero hizo na nyingine Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida Jeshi Lupembe alitangaza kumuondoa afisa mtendaji huyo katika kata hiyo huku Mbunge Sima akitoa majibu ya kero hizo kwa ufasaha.


Kabla ya kufanyika kwa mkutano huo Sima alitembelea na kukagua ujenzi wa madarasa manne ya sekondari ya kijiji hicho ambapo Sh. 80 Milioni zilipokelewa na ujenzi wake umekamilika sanjari na kununua madawati ambapo wanafunzi waliochaguliwa kuanza kidato cha kwanza watayatumia.


Aidha Sima alikagua ujenzi wa vyoo vya wanafunzi wa shule hiyo na kuagiza ukamilike kabla ya shule kuanza mapema wiki ijayo.


Baadhi ya wananchi waliopata fursa ya kutoa kero zao katika mkutano huo ni Samwel Kitiku, Richard Mangi, Hamisi Ramadhani, Ramadhani Mwanga, Juma Chimbe, Said Chima na Juma Orijoo.


Mbunge Sima anaendelea na ziara ya kutembelea kata zote na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na kufanya mikutano ya hadhara ili kujua changamoto walizonazo wananchi kwa lengo za kuzitafutia ufumbuzi.


No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso