LETENI WATOTO KATIKA UMOJA WA UTOTO MTAKATIFU ILI WAKUE KATIKA MAADILI,ASKOFU METHODIUS KILAINI - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Monday 2 January 2023

LETENI WATOTO KATIKA UMOJA WA UTOTO MTAKATIFU ILI WAKUE KATIKA MAADILI,ASKOFU METHODIUS KILAINI

Askofu akiwa na watawa

Mwonekano wa Kanisa jipya

Askofu akiwa na watjmishi wa misa pamoja na baadhi ya viongozi wazawa waishio mikoani

Msimamizi wa Kitume Jimbo Katoliki la Bukoba akiwa na watoto wa Utoto mtakatifu

MSIMAMIZI wa kitume wa Jimbo Katoliki la Bukoba,Askofu Methodius Kilaini,amewataka Wakatoliki kuwaruhusu watoto wao wadogo kujiunga na umoja wa utoto mtakatifu ili watoto hao waweze kulelewa kwa misingi ya dini kukuza imani zao,pia wakijifunza kusaidiana kwa kushirikiana na kushirikishana,ili hatimaye wawe raia wema wanaoweza kutumainiwa na kanisa na taifa kwa ujumla.

NA MUTAYOBA ARBOGAST-HUHESO BLOG-BUKOBA

Askofu Kilaini ameyasema hayo wakati akiongoza maadhimisho ya Misa Takatifu tarehe 28 Desemba 2022,katika Parokia Katoliki ya Kanyigo,siku ya utoto mtakatifu,na pia kutabaruku kanisa mama la Parokia,lililojengwa upya baada ya lile la zamani kubomolewa kupisha ujenzi.


Amewataka wazazi,walezi na jamii kwa jumla kulinda haki za watoto,kuwajali na kuwapenda ili waweze kufikia matamanio yao.


"Nafurahi kuwaona watoto wamejaa hapa wakifurahi pamoja nasi.Lakini hii haitoshi kama nyumbani hawana furaha.Basi tuwafanye watoto wetu kuwa na furaha kwa kuwatimizia mahitaji yao ya msingi",amesema Askofu.


Amekemea vitendo vya ukatili kwa watoto ikiwemo kutoa mimba na kutupa watoto,akirejea ukatili kwa watoto wadogo wa kiume chini ya miaka miwili waliouawa huko Bethlehemu (5 KK hivi) kwa agizo la mfalme Herode Mkuu (Math 2:16-18).


Akizungumzia juu ya kanisa jipya ambalo limejengwa kwa miaka tisa kwa gharama ya sh milioni 785,likiwa na uwezo wa kukaliwa na watu zaidi ya 1,000,Askofu amesifu juhudi za waumini wa Kanyigo,pamoja na wa madhehebu mengine,katika kutoa michango yao kufanikisha ujenzi huo hadi kanisa kukamilika,na sasa liko tayari kutumiwa.


"Kanisa si jengo tu,bali watu ndio kanisa,hivyo nawahimiza muwe watu wa sala na mlitumie kanisa hili kufikisha maombi yenu na kumshukuru Mungu" ,amesema


Amewahimiza waumini kuendelea kuchangia akisema kwa kawaida ujenzi huwa hauishi kwani bado kuna kazi ndogondogo za kung'arisha kanisa nk na hivyo kuagiza Kamati ya ujenzi inayoongozwa na bw.Richard Rweyemamu kutovunjwa.


Zaidi ya sh milioni 90 zinahitajika kwa mwaka 2023 kuendelea na shughuli mbalimbali katika makao makuu ya parokia hiyo.


Mkuu wa Parokia ya Kanyigo (Paroko), Padre Tatianus Kato amemshukuru Askofu mstaafu Desderius Rwoma ambaye pia amehudhuria maadhimisho hayo, aliyetoa baraka ujenzi huo uanze kwa kuweka jiwe la msingi, Askofu Methodius Kilaini kwa kuhudhuria Kanyigo Day kwa miaka yote tisa kuongoza harambee ya kuchangia ujenzi,Kamati tendaji ya Kigango cha Bugombe liliko kanisa mama na Kamati tendaji ya Parokia,Injinia padre Fulgence Rutatekururwa kwa shughuli za awali na mchoro wa kanisa,watendaji wakuu wa Kamati ya ujenzi (Richard Rweyemamu-Mwenyekiti,mhandisi Willibard Kombo-msimamizi ujenzi,Magreth Mugyabuso-mwekahazina) na watu wa madhehebu mengine,mapadre na walei kwa jumla.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso