MIPANGO YA SERIKALI KULETA NAFUU BEI YA GESI - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Tuesday, 7 October 2025

MIPANGO YA SERIKALI KULETA NAFUU BEI YA GESI








Serikali ya Tanzania imeongeza kasi ya juhudi zake za kupeleka gesi asilia kwa njia ya bomba moja kwa moja majumbani, ikisisitiza kuwa mradi huo ndio suluhisho la kudumu la kufanya nishati hiyo kuwa nafuu zaidi kwa Watanzania.




Wizara ya Nishati na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) zimeeleza wazi kuwa lengo kuu si kupunguza bei za mitungi ya gesi, bali ni kuondoa kabisa hitaji la mitungi hiyo kwa kuwekeza katika miundombinu ya bomba.




Kauli hiyo inatolewa huku Miradi ya kuunganisha gesi moja kwa moja majumbani inaendelea. Katika Jiji la Dar es Salaam, kwa mfano, TPDC inatekeleza mpango wa kuunganisha nyumba zaidi ya 1,000 na mtandao huo.




Juhudi hizi za Serikali za kusambaza gesi zinakwenda sambamba na ahadi zilizotolewa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya 2020-2025, ambayo inaitaja gesi asilia kama "injini ya maendeleo ya Tanzania" na chanzo cha nishati safi.




Aidha Katika baadhi ya maeneo kama Lindi, wateja wa awali wamepata fursa ya kuunganishiwa gesi bure ili kuondoa mzigo wa gharama kubwa za kuanzisha matumizi ya nishati hiyo.




Kwa mujibu wa Serikali, gesi asilia inayotumika kwa njia ya bomba huishia kuwa nafuu zaidi kuliko nishati nyingine, huku ikipunguza uharibifu wa mazingira unaotokana na matumizi ya kuni na mkaa.







Hata hivyo, kuelekea uchaguzi mkuu, kumekuwa na malalamiko mengi katika mitandao ya kijamii na mitaani yanayotaka Serikali itilie mkazo zaidi kwenye bei ya sasa ya gesi ya mitungi (LPG).




Wananchi wengi wamekuwa wakiomba bei za gesi, hasa mitungi midogo ya kujaza, ishuke hadi kufikia kiwango cha chini, wakisisitiza kuwa nchi yenye rasilimali nyingi za gesi haipaswi kuuza nishati hiyo kwa bei ghali kiasi hicho.




Serikali imesisitiza kuwa matumizi ya ndani yamepewa kipaumbele, na kiasi kikubwa cha gesi asilia (trilioni 1.3 kati ya futi za ujazo trilioni 57.54) kimetengwa kwa matumizi ya miaka mingi ijayo, na hivyo kuahidi mustakabali mwema wa nishati hiyo kwa Watanzania.




@@@@@@@@@@@@@@@@@




UCHAGUZI 2025: KUPIGA KURA NDIO 'SILAHA YA DEMOKRASIA'







Pamoja na Tanzania kuweka rekodi mpya ya kihistoria baada ya wapiga kura zaidi ya milioni 37.6 kujiandikisha kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 – idadi kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi,idadi hii kubwa inatajwa na wachambuzi kama ishara ya imani kubwa ya Watanzania katika mfumo wa kidemokrasia na amani.




Huku tarehe ya kupiga kura ikikaribia, Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) imethibitisha kuwa hamasa ya wananchi kushiriki katika kutimiza wajibu wao wa Kikatiba ni kubwa.




Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 5(1), inampa kila raia mwenye umri wa miaka 18 na zaidi haki ya msingi ya kupiga kura. Aidha Kauli za wananchi waliohojiwa zimeonyesha utambuzi wa kina wa umuhimu wa haki hii.




Mkazi wa Goba mkoani Dar es salaam,John James amesisitiza umuhimu wa kila mtu kushiriki: “Kupiga kura ni haki ya msingi. Ukikosa kupiga kura, unampa mwingine ruhusa ya kukuamulia kiongozi. Ni wajibu wetu kila mmoja kwenda kupiga kura kwa maendeleo ya nchi yetu.”




Khadija Suleiman, Mama Lishe kutoka Gongolamboto, anaelezea matarajio yake ya mabadiliko kupitia sanduku la kura: "Nitapiga kura Oktoba 29 kuchagua viongozi wanaojua shida za wananchi kama sisi. Tunataka viongozi wanaojali barabara, maji na mikopo kwa wanawake."




Kauli hizi zinadhibitisha kuwa Watanzania wanaona kura kama njia halali na ya amani ya kudai mabadiliko na maendeleo, na si kupitia maandamano, vurugu, wala jazba.




Tanzania: Nguzo ya Amani Afrika

Tanzania imejijengea heshima kubwa kimataifa kama mfano wa demokrasia barani Afrika, hasa kwa uwezo wake wa kuendesha chaguzi kwa amani, utulivu na utawala wa sheria.




Wachambuzi wa siasa wanasema kuwa dhamira hii ya Watanzania kutimiza wajibu wao kwa amani inathibitisha kuwa: "Watanzania hawatapigana; watapiga kura."




Kwa kuwa kura ni silaha muhimu ya kidemokrasia, Serikali na wadau wa demokrasia wamewataka Watanzania wote—vijana, wazee, wafanyabiashara, na wakulima—kujitokeza kwa wingi Oktoba 29, kupiga kura kwa utulivu, na kisha kurudi majumbani kwa heshima ya taifa.




Kura yako ni sauti yako. Sauti yako ni nguvu ya taifa. Usiiache.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso