WAANDISHI HABARI WAHIMIZWA KUENDELEA KUANDIKA JUU YA HABARI ZA MARBURG NA KUZUIA UNYANYAPAA NA UBAGUZI KWA WAATHIRIKA - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Saturday 10 June 2023

WAANDISHI HABARI WAHIMIZWA KUENDELEA KUANDIKA JUU YA HABARI ZA MARBURG NA KUZUIA UNYANYAPAA NA UBAGUZI KWA WAATHIRIKA

Imeelezwa kuwa, kutangazwa kwa kwisha kabisa kwa mlipuko wa ugonjwa wa Marburg mkoani Kagera, hakuna maana kwamba waandishi habari hawana kazi tena kuandika juu ya ugonjwa huo, bali ndipo wazidishe juhudi katika kuwaelimisha watu njia za kujikinga na milipuko mingine ya magonjwa namna hiyo, na pia kuzuia unyanyapaa na ubaguzi kwa waathirika.

Na Mutayoba Arbogast, HUHESO DIGITAL BLOG, Bukoba


Kutoka kshoto waliokaa,Livinstone Byekwaso wa shirika la KAMEA, Rev. Dr Godfey Aligawesa, Mkurugenzi mtendaji wa Redio Karagwe na Mganga mkuu wa wilaya ya Karagwe, Agnes Mwaifuge pamoja na waandishi wa habari

Hayo yamebainishwa na Mganga mkuu wa wilaya ya Karagwe(DMO), Dr Agnes Mwaifuge tarehe 8 Juni 2023, wakati akiwasilisha mada ya Dhana ya Unyanyapaa na Ubaguzi kwa waathirika wa magonjwa ya mlipuko, kwenye mafunzo ya siku moja kwa waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari mkoani Kagera, mafunzo yaliyoratibiwa na Redio Karagwe 91.4 FM ambayo ni redio ya kijamii wilayani Karagwe mkoa wa Kagera.


Mkurugenzi mtendaji wa Kituo hicho cha redio, Mchungaji, Dr Godfrey Aligawesa, amelishukuru Shirika la Kimataifa la kuhudumia watoto duniani (UNICEF) , kwa kuyasaidia mashirika mengine kuweza kuendesha elimu ya kujikinga na ugonjwa wa Marburg na kupinga unyanyapaa na ubaguzi kwa wahanga wa ugonjwa huo na familia zao.


Amesema kituo chake ni mwanachama wa Mtandao wa redio za kijamii hapa nchini(TADIO)uliowezeshwa na UNICEF, hivyo nao Redio Karagwe wamenufaika na msaada huo.


Dr Mwaifuge amesema ziko athari kadhaa iwapo waathirika watanyanyapaliwa na kutengwa kwani wanaweza kukata tamaa na 'kujikataa' na hivyo kufanya suala la kurejesha afya zao kuwa gumu, na hata kuenea kwa maambukizi zaidi iwapo kuna mlipuko mwingine.


"Tuandike habari zinazoelimisha jamii na kuwatia moyo famila za wahanga wa Marburg watambue kwamba huo ni ugonjwa kama yalivyo mengine tusiwanyanyapae kwani tukiwabagua inaweza kusababisha madhara kama vile kuwajengea hofu,kuwakatisha tamaa,kujiona kuwa wao hawafai na kujiua", anaeleza Mwaifuge.


Ameongeza kusema kuwa, kutowabagua wagonjwa wa magonjwa yoyote yanapotokea katika jamii hususani ya mlipuko itasaidia watu kutoa taarifa, kupima, kupata matibabu, kupunguza maambukizi na kuwa huru hivyo akawashauri waandishi wa habari kuwasiliana na waathirika hao ili kuandika habari kwa umakini na weledi, katika kujua maendeleo na changamoto zao bila kuleta taharuki kwa umma na penye mashaka wasisite kuwasiliana na wataalam wa afya.


Jumla ya watu tisa katika kata za Kanyangereko na Maruku wilayani Bukoba walithibitishwa kuwa na maambukizi, huku sita wakipoteza maisha na watatu kunusurika.


Juni 02,2023 Waziri wa afya Ummy Mwalimu alilitangazia Taifa na Jumuiya za kimataifa afya kumalizika ugonjwa huo mkoani Kagera,ikithibitishwa pia na Shirika la afya ulimwenguni (WHO).

Mganga mkuu wa Wilaya ya Karagwe(aliyesimama), Agnes Mwaifuge akiwasilisha mada kwa waandishi habari kuzuia unyanyapaa na ubaguzi kwa waathrika wa magonjwa hususan Marburg

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso